RSS
Nchi za Kiislamu zinapaswa kuimarisha umoja wa Waislamu na kutetea haki zao (2010/03/04 - 16:03)

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran Ayatullah Ali Khamenei leo amekutana na viongozi wa serikali na wananchi wa matabaka mbalimbali kwa mnasaba wa kuadhimisha Maulidi ya Mtume wa nuru, uadilifu na rehma Muhammad (saw) na mjukuu wake Imam Ja'far Swadiq (as). Ayatullah Khamenei amesisitiza katika hadhara hiyo kwamba kuzalisha upya hakika na maarifa ya Kiislamu na kutekeleza mafundisho ya Mtume wa Mwisho wa Mwenyezi Mungu ndiyo haja kubwa zaidi ya umma wa Kiislamu. Amesema kuwa umoja na mshikamano wa wafuasi wa madhehebu mbalimbali za Kiislamu ndio wenzo wa kutatua matatizo mbalimbali na sababu ya maendeleo na ustawi wa ulimwengu wa Kiislamu.

Katika hadhara hiyo ambayo imehudhuriwa pia na viongozi wa ngazi za juu wa mfumo wa Kiislamu hapa nchini, mabalozi wa nchi za Kiislamu, wageni, maulamaa na wanafikra wa Kiislamu walioshiriki kwenye Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu uliomalizika leo mjini Tehran, Ayatullah Ali Khamenei amewapa Waislamu wote mkono wa baraka na fanaka kwa mnasaba wa Maulidi na kuzaliwa kiini cha matukufu yote ya Mwenyezi Mungu na Nabii Mteule Muhammad bin Abdullah (saw) na wasii wake wa kweli, muenezaji wa Uislamu halisi Imam Ja'far Swadiq (as) na akasema: "Matukufu yote ya kibinadamu na maadili mema yametokana na kuzaliwa kutukufu kwa Mtume katika giza kubwa la ujinga, upotovu na mghafala.

Amesema umma wa Kiislamu unahitajia mno kutafakati na kusoma upya mafundisho na uongofu wa Mtume wa Mwisho (saw). Ameashiria jamii kubwa ya umma wa Kiislamu, nafasi nzuri ya kijiografia, utajiri mkubwa, vipawa na uwezo wa kibinadamu vya ulimwengu wa Kiislamu na akahoji kwamba, kwanini ulimwengu wa Kiislamu ukawa katika hali ya mparaganyiko na kusumbuliwa na matatizo mengi kama ufukara, ubaguzi, kubakia nyuma kielimu na udhaifu wa kiutamaduni licha ya kuwa na sifa hizo adhimu, na wala hauwezi kutetea haki zake mbele ya madhalimu wa ulimwengu?

Akibainisha udhaifu wa ulimwengu wa Kiislamu na kutoweza kwake kutetea haki za Waislamu, Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu ametolea mfano kadhia ya Palestina na akasema kughusubiwa ardhi ya kihistoria na takatifu ya Palestina na dhulma isiyokuwa na kikomo na ya siku zote ya Wazayuni watenda jinai dhidi ya taifa linalodhulumiwa la Palestina ni jeraha kubwa linalousumbua mno mwili wa umma wa Kiislamu; lakini ulimwengu wa Kiislamu unaamiliana na kadhia hiyo kana kwamba suala la Palestina haliuhusu.

Ayatullah Ali Khamenei amelitaja dola bandia na la Kizayuni la Israel kuwa ni donda hatari la saratani na akaongeza kuwa njia pekee ya kujilinda mbele ya saratani hiyo angamizi na waungaji mkono wake ni kurejea kwenye Uislamu na kuyapa umuhimu mafundisho ya Mtume Mtukufu wa dini hiyo.

Vilevile amefafanua sababu za kushindwa ulimwengu wa Kiislamu katika kutetea haki za wafuasi wa dini hiyo akiashiria njama za mara kwa mara za Marekani, Uingereza na maadui wengine wa Uislamu katika kuzusha hitilafu na mfarakano katika umma na akasema: "Madhalimu hao mabeberu wanaelewa vyema kwamba hitilafu na migawanyiko inaufanya umma wa Kiislamu uwe mbali na kadhia muhimu mno ya Palestina, kwa sababu hiyo wanatumia kila linalowezekana kuchochea moto wa mifarakano ya kikabila, kimadhehebu na kijiografia katika nyoyo za Waislamu wa Shia na Suni na wafuasi wa madhehebu nyingine za Kiislamu.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa haja nyingine kubwa ya umma mkubwa wa Kiislamu ni kujenga upendo na umoja na ametoa wito kwa serikali, wanafikra, maulamaa, wanahakati wa masuala ya kisiasa na kijamii wa nchi za Kiislamu kutekeleza wajibu wao wa kuimarisha umoja na mshikamano. Amesema iwapo mwamko wa Kiislamu utapanuka na kuimarika zaidi, na nyoyo za Waislamu zikakurubiana zaidi na zaidi, njia ya kuamiliana, ushirikiano na maendeleo ya Waislamu wote itafunguliwa na matatizo mengi ya ulimwengu wa Kiislamu likiwemo suala la Palestina, yatapatiwa ufumbuzi.

Ayatullah Khamenei amesema kuwa madhehebu zote za Kiislamu zinakubaliana kwamba ni wajibu kulinda na kutetea ardhi za Kiislamu zinazoshambuliwa na kuvamiwa. Ameongeza kuwa hata hivyo na licha ya kuwa na mtazamo wa aina moja kuhusu kadhia hiyo, inasikitisha kwamba ulimwengu wa Kiislamu umeathiriwa na njama za Marekani na Uingereza za kuzusha mifarakano na hitilafu kati ya Shia na Suni na madhehebu nyingine za Kiislamu.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema moja ya malengo yanayopewa kipaumbele na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni umoja wa Waislamu na kutetea kadhia ya Palestina. Amekumbusha maneno ya hayati Imam Ruhullah Khomeini na sisitizo lake juu ya umoja na mshikamano wa Kiislamu na kadhia ya Palestina na akasema: "Mfumo wa Kiislamu wa Iran, viongozi wote wa nchi na taifa kubwa la Iran linayatambua masuala hayo ya kimsingi kuwa ni wajibu wake wa kisheria na kidini na kauli na msimamo wao wote ni mmoja katika masuala hayo."

Ameongeza kuwa mwamko unaoongezeka kila siku wa umma wa Kiislamu na sauti za mataifa mbalimbali za kutetea Plestina ni mwangwi nzuri wa misimamo ya haki ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika fikra za watu wa ulimwengu wa Kiislamu. Ayatullah Khamenei amesema: "Nchi za Kiislamu pia zinapaswa kumfuata Mtume Mtukufu kwa kuimarisha umoja wa Waislamu na kutetea haki zao hususan katika kukabiliana na donda la saratani yaani Israel ghasibu na waungaji mkono wake, ili umma wa Kiislamu uweze kufikia maendeleo na ufanisi wa dunia na akhera kwa msaada wake Mola Muweza.

Mwanzoni mwa mkutano huo Rais Mahmoud Ahmadinejad wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aliwapongeza Waislamu wote kwa mnasaba wa Maulidi na maadhimisho ya siku ya kuzaliwa Mtume wa upendo na mahaba na mjumbe wa elimu na hikima na akasema: "Jamii ya sasa ya mwanadamu inahitajia zaidi maarifa na mfumo wa Mtume wa Mwisho Muhammad (saw) kuliko wakati wowote mwingine ili kuweza kuangamiza ujahili na ubeberu, ukatili na kuwadunisha watu na hitilafu na ubaguzi na hatimaye vipawa vya mwanadamu kote ulimwenguni vipate fursa ya kuchanua kwa kusimamishwa uadilifu.

Dakta Ahmadinejad amezungumzia pia ujumbe unaompa mwanadamu saada na ufanisi wa kuzaliwa Mtume wa Mwisho Muhammad amani ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake na Ali zake na akaongeza kuwa baada ya ushindi wa Mapinduzi adhimu ya Kiislamu, taifa la waumini la Iran lilishika bendera ya kupigania haki na uadilifu na litaendeleza njia hiyo kwa umoja na mshikamano wa Waislamu.

Mwishoni mwa mkutano huo, maulamaa na wanafikra wa Kiislamu walioshiriki katika Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu walifanya mazungumzo na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi katika anga ya kirafiki na kidugu.